Gazeti huru

Soma habari zenye uhakika
Powered by Blogger.

Latest Post

CCM yaibuka kidedea Kata ya Mrijo

Written By Unknown on Friday, February 14, 2014 | 2:02 AM

MwanaCCM hai kutoka Jamhuri ya Watu wa China
Na Khamis Mkotya

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimepata ushindi mkubwa katika uchaguzi mdogo Kata ya Mrijo, Wilaya Chemba, mkoani Dodoma.

Katika uchaguzi huo uliofanyika juzi, mgombea wa chama hicho, Khamis Msakati, alishinda kwa kura 1,261 na kuwashinda vibaya wapinzani wake.

Akitangaza matokeo hayo juzi usiku, Msimamizi Msaidizi wa Uchaguzi huo, Khamis Mwande, alisema Msakati alipata kura hizo kati ya kura halali 2,430 zilizopigwa.

Katika uchaguzi huo, Msakati alifuatiwa na mpinzani wake wa karibu, Said Kibinda (CUF), aliyepata kura 904, Omary Guka (Chadema) kura 248, huku mgombea wa NCCR-Mageuzi, Awadi Msuka, akiambulia kura 17.

“Tulitangaza matokeo saa 2:15 usiku, baada ya matokeo yote kufika katika kituo cha kujumlishia katika Kijiji cha Mrijo Chini. Kulikuwa na vituo 19 katika vijiji sita vinavyounda Kata ya Mrijo.

“Kimsingi tunashukuru uchaguzi umefanyika vizuri tangu kipindi cha kampeni hadi juzi tulipopiga kura hapakuwa na vurugu zozote, tumesikia sehemu nyingine watu wamekatana mapanga, lakini hapa Mrijo hali ilikuwa shwari.

“Wagombea wote walikubali kusaini fomu ya matokeo, ingawa mgombea wa NCCR-Mageuzi hakuweza kusaini, kwani aliingia mitini mwenyewe baada ya kuona ameshindwa vibaya,” alisema.

Kwa mujibu wa Mwande, wananchi waliotarajiwa kupiga kura katika kata hiyo walikuwa 7,434, lakini waliojitokeza walikuwa 2,448. Kura 18 kati ya hizo ziliharibika.

“Kwa takwimu hizo utaona takriban watu 5,000 hawakujitokeza kupiga kura. Sababu yake ni moja tu, huu ni msimu wa kilimo, watu wengi wapo mashambani,” alisema.

Msakati alisindikizwa kwa shamrashamra na nderemo kutoka eneo la ofisi za kata hadi nyumbani kwake, eneo la Chang’ombe, mara baada ya kukabidhiwa cheti cha ushindi.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Chemba, Al-haj Shaaban Kilalo, aliwashukuru wananchi wa Mrijo kwa kuendelea kuwa na imani na CCM na kusema kuwa hizo ni salamu kwa vyama vya upinzani.

Uchaguzi huo ulifanyika kujaza nafasi iliyoachwa wazi na aliyekuwa diwani wa kata hiyo, Halifa Nyasuka (CCM), aliyefariki dunia Juni 15 mwaka jana, kutokana na maradhi ya kichwa.

Uchaguzi huo ni sehemu ya uchaguzi mdogo uliofanyika katika kata 27 nchini kote, kama ilivyotangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).

JK kuhudhuria mkutano wa ujangili London

Vijana wa Yanga wakiwa katika maandalizi ya kibano
Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

RAIS Jakaya Kikwete ameteuliwa kutoa mada katika mkutano maalumu wa kupambana na tatizo la ujangili duniani, unaotarajiwa kufanyika mjini London, Uingereza wiki hii.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dar es Salaam jana, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, alisema mkutano maalumu umeandaliwa na Mwanamfalme wa Uingereza, Prince Charles.

Alisema mkutano huo, utajikita zaidi kujadili tatizo la ujangili kwa wanyama kama tembo, faru na chui, ambao wamekuwa wakiuawa usiku na mchana.

“Rais Kikwete ameteuliwa katika jopo kubwa la viongozi kutoa mada juu ya tatizo la ujangili, hii ni heshima kubwa mno kwetu sisi ambao tumekuwa tunapambana na tatizo hili kila kukicha.

“Mkutano huu umekuja wakati ambao kuna vita kali ya ujangili wa tembo na faru, wanazidi kuuawa, tunaamini katika mkutano huu tutakuja na njia mpya ambayo itatusaidia kukabiliana na tatizo hili,” alisema Waziri Nyalandu.

Alisema juzi gazeti la Daily Mail la Uingereza liliandika habari za upotoshaji mkubwa kwamba Serikali ya Tanzania haijachukua hatua zozote za kukabiliana na ujangili.

“Tumesikitishwa na habari za upotoshwaji mkubwa uliofanywa na gazeti hili, eti linasema Tanzania haijafanya kazi yoyote ya kupambana na ujangili, nawahakikishia kazi imefanyika kwa nguvu kubwa mno, ninyi nyote ni mashahidi.

“Naomba ielewekwa kwamba shehena zote zilizokamatwa ndani na nje ya nchi ni juhudi za Serikali ikishirikiana na polisi wa kimataifa (Interpol), ambao wamekuwa wakifanya kazi kwa karibu na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama.

“Tunapenda kuiarifu dunia kuwa katika kipindi cha kutoka mwaka 2010-13, jumla ya kilo 19,943, sawa na tani 20 za meno ya tembo zilikamatwa nchini, watuhumiwa 322 walikamatwa na kufikishwa mahakamni.

“Mwaka 2013 peke yake, tani 12.2 za meno zilikamatwa na watuhumiwa 145 walitiwa mbaroni, akiwamo raia wa Uingereza, Robert Dewar Twist, ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Trans Africa Logistic Limited ya Dar es Salaam,” alisema Waziri Nyalandu.

Alisema kwa takwimu hizo, ni wazi Serikali imeonyesha namna ambavyo inapambana vikali na tatizo hilo.

Alisema vita dhidi ya ujangili ni kali na ina mtandao mkubwa wa siri kutoka nje ya nchi, lakini Serikali imejipanga vya kutosha kukabiliana nao.

Madabida kortini kwa ARV feki

Aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Kagasheki
Na Kulwa Mzee, Dar es Salaam

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhani Madabida na wenzake watano wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kwa tuhuma za kusambaza dawa feki za ARV’s na kujipatia Sh milioni 148 kwa njia ya udanganyifu.

Madabida na wenzake, walipanda kizimbani jana mbele ya Hakimu Mkazi Nyigulile Mwaseba na kusomewa mashtaka matano na Wakili wa Serikali, Shadrack Kimaro.

Kimaro alidai shtaka la kwanza, linamkabili mshtakiwa Madabida (Ofisa Mtendaji Mkuu), Seif Shamte (Mkurugenzi wa Uendeshaji), Simon Msoffe (meneja masoko) na mshtakiwa wa nne, Fatma Shango (mhasibu msaidizi) wa Tanzania Pharmaceutical Industries Ltd.

Alidai washtakiwa hao, wanadaiwa Aprili 5, 2011 jijini Dar es Salaam waliisambazia Bohari Kuu ya Dawa kopo 7,776 za dawa bandia za ARV’s zenye mchanganyiko wa dawa ya stavudin 30mg +nevirapine 200mg+lamivudine 150mg.

Dawa hizo zilizotengenezwa Machi, 2011 na kuisha muda wake wa matumizi Februari, 2013 zilionyesha kuwa ni halali wakati si kweli.

Shtaka la pili kwa washtakiwa hao, wanadaiwa kuisambazia Bohari Kuu ya Dawa (MSD) kopo 4,476 na shtaka la tatu wanashtakiwa kwa kujipatia Dola za Marekani 98,506.08 (sawa na Sh 148,350,156 za Tanzania kwa udanganyifu, baada ya kuonyesha kwamba fedha hizo ni malipo ya makopo 12,252 ya dawa hizo za ARV’s.

“Mheshimiwa hakimu, shtaka la nne linamkabili mshtakiwa wa tano, Sadick Materu na mshtakiwa wa sita, Evans Mwemezi ambao wanadaiwa kati ya Aprili 5 na 13, mwaka 2011 wakiwa maofisa wa Bohari Kuu ya Dawa, walishindwa kuzuia kosa kutendeka.

“Shtaka la tano, linawakabili washtakiwa wote, mnadaiwa katika kipindi hicho mlishindwa kutimiza wajibu na kuisababishia Bohari ya Dawa hasara ya Sh 148,350,156.48,” alisema.

Washtakiwa walikana kutenda makosa hayo, upande wa Jamhuri haukuwa na pingamizi kwa washtakiwa kupewa dhamana, isipokuwa waliiomba mahakama kuzingatia sheria kwa kuangalia thamani ya fedha wanazodaiwa kujipatia washtakiwa.

Hakimu Mwaseba, aliwataka washtakiwa kuwa na wadhamini wawili watakaosaini dhamana ya Sh 6,181,256 kila mmoja, wawe wafanyakazi wa taasisi inayotambulika na kila mshtakiwa anatakiwa kuweka fedha taslimu au hati ya mali isiyohamishika yenye thamani ya Sh 12,362,513.

Washtakiwa wote, walitimiza masharti ya dhamana na mahakama iliwakubalia hadi kesi yao itakapotajwa tena kwa sababu upelelezi haujakamilika.

Jengo linalochungulia Ikulu kubomolewa

Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joesph Warioba
Na Kulwa Mzee, Dar es Salaam

MKURUGENZI Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA), Makumba Kimweri na Msanifu Mkuu, Richard Maliyaga wametiwa hatiani kwa kutumia madaraka vibaya, kwa kutoa kibali cha ujenzi wa ghorofa 18 jirani na Ikulu kinyume na utaratibu.

Mahakama imeamuru ghorofa kuanzia ya saba hadi ya 18, zibomolewe kwani haziko halali kutokana na matumizi ya eneo hilo.

Washtakiwa hao, walitiwa hatiani na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mjini Dar es Salaam jana mbele ya Hakimu Mkazi, Sundi Fimbo baada ya kupitia ushahidi na kuridhika kwamba washtakiwa walitenda makosa hayo.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Fimbo alisema washtakiwa walishtakiwa kwa makosa matano ya matumizi mabaya ya ofisi katika utoaji kibali cha ujenzi wa jengo la ghorofa 18 katika kiwanja namba 45 na 46 Mtaa wa Chimara.

“Mahakama imepitia ushahidi na kujiridhisha kwamba washtakiwa walitenda makosa hayo, hivyo wanatiwa hatiani kwa makosa yote matano.

“Mshtakiwa Kimweri, anatiwa hatiani kwa kosa la kwanza, la pili na shtaka la tano na mshtakiwa Maliyaga anatiwa hatiani kwa shtaka la tatu, nne na tano.

“Kutokana na mashtaka yanayowakabili washtakiwa, mahakama inawahukumu kwenda jela miaka mitatu kwa kila kosa au kulipa faini ya Sh milioni tano kwa kila kosa,” alisema.

Kutokana na hukumu hiyo, washtakiwa wanatakiwa kwenda jela miaka tisa na kulipa faini ya jumla ya Sh milioni 15.

“Jengo lilitakiwa liwe la ghorofa sita, hivyo mahakama inaamuru kuanzia ghorofa ya saba hadi 18 zibomolewe, naishangaa Manispaa ya Ilala kwanini haikuondoa ghorofa zilizozidi wakati sheria inawaruhusu,” alisema Hakimu Fimbo.

Hata hivyo, washtakiwa walinusurika kwenda jela baada ya kulipa faini waliyopangiwa na mahakama. Jengo hilo linamilikiwa kwa ubia kati ya Kampuni ya Royalle Orchard Inn na TBA.

Awali akiwasomea mashtaka, Wakili wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Leonard Swai alidai Agosti 6, 2007, Kimweri akiwa Mtendaji Mkuu wa TBA kwakutumia vibaya madaraka yake, alisaini hati ya makubaliano yenye namba TBA/JVA/DSM/ROI/001 kati ya TBA na Kampuni ya Royalle Orchard Inn Ltd, akiwa na lengo la kuanzisha ujenzi na wamiliki binafsi wa umma wa ghorofa 15, kwenye Kitalu namba 45 katika Mtaa wa Chimara, Wilaya ya Ilala bila eneo hilo kufanyiwa upembuzi yakinifu.

Alidai katika tarehe hiyo, Kimweri alitumia vibaya madaraka kwa kusaini hati ya makubaliano namba TBA/JVA/DSM/ROI/002 kati ya TBA na kampuni hizo akiwa na lengo la kuingia ubia kati ya Serikali na kampuni binafsi (PPP) wa ghorofa 15, kwenye Kitalu namba 46 eneo la Chimara bila kufanya upembuzi yakinifu katika mradi huo na kuipatia faida Kampuni ya Royalle Orchard Inn Ltd.

Alidai Julai 21, 2008, mshitakiwa Richard ambaye ni Msanifu Mkuu kwa kutumia vibaya madaraka yake, alitoa hati namba TBA/BP/155 na kuruhusu Kampuni ya Royalle Orchard Inn Ltd, kujenga ghorofa 15 za biashara kwenye Kitalu namba 45 na 46 bila ridhaa ya Mipango Miji ya Manispaa ya Ilala na kuipatia faida kampuni hiyo.

Pia alidai Aprili 9, 2009, Richard kwa kutumia madaraka yake vibaya, aliruhusu Kampuni ya Royalle Orchard Inn Ltd kujenga ghorofa 15 hadi 18 za biashara katika Mtaa wa Chimara, Kitalu cha 45 na 46 bila ridhaa husika ya Mipango Miji ya Manispaa ya Ilala na kuipatia kampuni hiyo faida.

Katika shtaka la mwisho, washtakiwa wote kwa pamoja walidaiwa katika tarehe tofauti katika ofisi za TBA, Kimweri akiwa Mtendaji Mkuu na Richard akiwa Msanifu Mkuu, katika utekelezaji wa kazi zao, walitumia vibaya madaraka kwa kuiruhusu Kampuni ya Royalle Orchard Inn Ltd kujenga jengo la biashara bila kupata ruhusa kwa ajili ya mabadiliko ya matumizi.
 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. Jambo Leo - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger